Top Ad 728x90

Tuesday 1 March 2016

Kaburi la Halaiki la Maiti zaidi ya 30..Lapatikana Burundi



Maafisa wa polisi na utawala wa mji mkuu wa Bujumbura Burundi wamegundua kaburi la halaiki linaloshukiwa kuwa na takriban miili 30.

Mwandishi wa BBC aliyeko huko Prime Ndikumagenge anasema kuwa miili 3 na fuvu la kichwa ilipatikana katika eneo la Mutakura Kaskazini mwa Bujumbura.

Kitongoji hicho cha Mutakura ni moja ya ile iliyosheheni wafuasi wa upinzani ambao walijitokeza mabarabarani wakiandamana kupinga kauli ya rais Pierre Nkurunziza kuwania muhula wa tatu uongozini.

Nkurunziza alitangaza nia ya kuwania muhula wa tatu mwezi Aprili mwaka uliopita kinyume cha katiba akidai kuwa mhula wa kwanza hakuchaguliwa na umma.

 Wapinzani wake hata hivyo wanadai kuwa alikiuka katiba ya taifa.

Meya wa mji wa Bujumbura Freddy Mbonimpa anasema walipokea habari hiyo kutoka kwa ''wahuni waliojisalimisha kwa utawala''.

Haikuelezwa kwa hakika waliuawa lini au na nani na nani aliyewazika pahala hapo.
Meya huyo hata hivyo alidai kuwa waliopatikana wameuawa walikuwa ni wafuasi wa rais Nkurunziza.

Kuwepo kwa makaburi ya halaiki kuligunduliwa kwanza na kundi linalopigania haki za kibinadamu la Amnesty International mwezi Januari.

Ripoti hiyo ya kundi la kutetea haki za binadamu la lilichapishwa tarehe 11 Desemba mwaka uliopita siku moja baada ya serikali kukiri kuwa wamewaua watu 79 na kupoteza maafisa 8 wa polisi.

Meya huyo leo amekiri kuwa utawala wake ulizika miili ya watu 58 katika makaburi ya halaiki katika makaburi yanayofahamika.

Umoja wa Mataifa unasisitiza kuwa zaidi ya watu 430 waliuawa nchini Burundi tangu kauli ya rais Nkurunziza kubainika mwezi Aprili.

0 comments:

Post a Comment

Top Ad 728x90